TBD
Hapa na pale
Vikosi vya Uangalizi vya UM katika Georgia (UNOMIG) vimesitisha rasmi shughuli zao kuanzia tarehe 16 Juni 2009, baada ya Baraza la Usalama liliposhindwa kupitisha azimio la kuongeza muda wa operesheni hizo. Wanajeshi wa UNOMIG wameshaanza kuondoka Georgia kwa hivi sasa. Taarifa ya KM iliyashukuru makundi husika kwa ushirikiano wao na vikosi vya UNOMIG tangu pale vilipoanza operesheni zake katika 1993. KM alisema UM upo tayari kutumika kwenye shughuli nyenginezo za kuimarisha amani katika Georgia. Kwa kulingana na pendekzo hilo KM amemtaka Mjumbe Maalumu wake anayehusika na UNOMIG, Johan Verbeke kuendelea kuiwakilisha UM kwenye majadiliano ya Geneva yanayozingatia usalama na ututlivu wa eneo husika, mazungumzo yanayozingatia pia suala la kuwarudisha makwao wahamiaji waliopo nje na wale wa ndani ya nchi.
Kai Eide, Mjumbe Maalumu wa KM kwa Afghanistan aliwaambia wajumbe wa Baraza la Usalama waliokutana asubuhi, kwenye kikao cha hadhara, ya kwamba hali katika Afghanistan hivi sasa imekabiliwa na utata mkubwa. Lakini Eide alisema anaamini pindi hali itadhibitiwa kama inavyotakikana kuna matumaini ya Afghanistan kuanzisha kipindi muhimu cha mabadiliko yatakayokomesha kabisa mapigano na kudumisha amani nchini. Alisema uchaguzi unaotarajiwa kufanyika mwezi Agosti, ukifanikiwa, una uwezo wa kusaidia kurudisha tena imani miongoni mwa raia juu ya uthabiti wa mfumo wa kidemokrasia katika kuimarisha taasisi za utawala katika Afghanistan, kwa ujumla. Aliyanasihi makundi yote ya kisiasa na wagombea uchaguzi kujitahidi kuendeleza kampeni zao kwa hishima na usawa, na kwa natija za wazalendo wote. Vile vile Eide aliitahadharisha jamii ya kimataifa kutoingilia kati, asilan, utaratibu wa aina yoyote ule unaotumiwa kuendesha shughuli za uchaguzi katika Afghanistan.
Siku ya Ujumanne, tarehe 30 Juni 2009 ni siku ya mwisho kwa Uraisi wa Uturuki kwenye Baraza la Usalama. Kuanzia Ijumatano, tarehe 01 Julai 2009, Uganda itakabidhiwa Uraisi wa duru wa Baraza la Usalama, na kuongoza shughuli zake kwa mwezi Julai.
Mjumbe Maalumu wa KM kwa Iraq, Staffan de Mistura, leo amemaliza muda wa kazi na anajitayarisha kuondoka kurejea Sweden. Aliipongeza Serikali ya Iraq kwa kuonyesha moyo wa kutia moyo kwa kuwakilisha maendeleo ya kiawamu, hasa kwenye zile juhudi za kurudisha uhuru kamili wa taifa, na katika kuhakikisha Iraq itakuwa ni taifa lilioungana, lenye mfumo wa kidemokrasia na tulivu. Alisema tarehe ya leo inawasilisha pia siku muhimu ya kihistoria, kitaifa, taifa baada ya vikosi vya Marekani kuondoshwa kutoka miji ya Iraq na kuhamishwa kwenye kambi za kijeshi zilitawanywa katika sehemu mbalimbali za nchi.
Ofisi ya Mpatanishi Mkuu wa Pamoja wa UM-UA kwa Darfur imetangaza taarifa iliosema makundi ya waasi wa Darfur yapo tayari kurudia mazungumzo ya amani na Serikali ya Sudan. Kwa mujibu wa taarifa hiyo Mpatanishi wa UM-UA juu ya Darfur, Djibril Bassolé mapema Ijumanne alikutana na viongozi wa waasi kwenye mji wa Tripoli, Libya na alishauriana nawo juu ya mazungumzo ya amani ya Doha, na namna makundi ya upinzani yatakavyoshiriki kwenye juhudi za kusuluhisha mgogoro uliokabili eneo lao.
Vikosi vya Mchanganyiko vya UM-UA kwa Darfur (UNAMID) vimeripoti baadhi ya wanajeshi wake walishambuliwa Ijumatatu karibu na kambi ya Geneina, katika Darfur Magharibi. Mwanajeshi mmoja alipata jeraha la risasi na hali yake inaripotiwa kuwa tulivu. Washambulizi wa tukio hilo bado hawajatambuliwa. Vile vile UNAMID imeripoti vikosi vya mwanzo vya majeshi ya kulinda amani kutoka Ethiopia vimewasili Darfur baada ya safari ya barabara iliokamilisha kilomita 1,800.

