Pillay aisifu Indonesia kwa kuridhia mikataba ya haki za binadamu lakini ataka itekelezwe nyumbani
Kusikiliza /
Kamishna Mkuu wa Haki za Binadamu katika Umoja wa Mataifa, Navi Pillay, ameisifu serikali ya Indonesia kwa kuridhia mikataba ya kimataifa ya haki za binadamu haraka, na wakati huohuo kuitaka itekeleze mikataba hiyo nyumbani.
Bi Pillay, ambaye amekuwa kwenye ziara rasmi nchini Indonesia tangu Jumapili, amesema kuwa ameridhishwa kwa kuona kuwa harakati za kuzitafsiri sheria hizo za kimataifa katika muktadha wa sheria za Indonesia zimeanza katika maeneo mengi ya taifa hilo, na kuisihi serikali isirudi nyuma katika juhudi hizo.
Licha ya hayo, Bi Pillay ameelezea kusikitishwa kwake na kuwepo viwango vya juu vya ubaguzi wa kijinsia dhidi ya wanawake, na dhuluma dhidi ya watu wanaolazimishiwa sheria ya dini ya Kiislamu, hasa katika jimbo la Aceh.
