Tayari mabadiliko yameanza kuonekana Somalia: Mahiga
Kusikiliza /Mwakilishi maalum wa Umoja wa Mataifa kuhusu Somalia, Augustine Mahiga, amesema nchi ya Somalia tayari imeanza kushuhudia mabadiliko muhimu, kufuatia kuundwa kwa bunge na uchaguzi wa rais hivi karibuni, ambao amesema ulikuwa mojawapo wa kidemokrasia zaidi barani Afrika.
Akizungumza na waandishi wa habari mjini Nairobi, Bwana Mahiga amesema hali ya usalama katika mji mkuu wa Mogadishu imeanza kuimarika, na mitaa yake kuanza kushuhudia biashara na uwekezaji kwa viwango vya juu. Ameongeza kuwa badala ya milio ya risasi, zinasikika sasa sauti za nyundo za ujenzi.
Amesema kuwafurusha wanamgambo wa Al-Shabaab kutoka mji wa Kismayo ni mojawapo ya mafanikio ambayo yamepatikana, tangu kuundwa serikali mpya. Amesema mlango uliachwa wazi ili Al-shabaab wajiunge kwenye serikali, lakini hawakutaka. Ametoa wito kwa rais mpya wa Somalia amteue Waziri Mkuu kabla ya tarehe 10 Oktoba na aidhinishwe na bunge, ili kukamilisha harakati zote za kuunda serikali mpya.
